Uwazi wa Mikataba katika Sekta ya Uziduaji (Mafuta, Gesi na Madini)

Roving Journalist

JF Roving Journalist
Apr 18, 2017
2,796
11,959
Serikali inapokubaliana na makampuni binafsi katika kuchimba maliasili wananchi huwa na haki ya kujua kile kilichokubaliwa.

ANGALIA VIDEO:



Meneja wa kampeni Oxfam, Jovita Mlay anasema: “Serikali imeingia kwenye mikataba kadhaa kwenye sekta ya Uziduaji lakini wananchi hawajui ni kitu gani kipo kwenye hiyo mikataba.”

Kikatiba inaelezwa kwamba wananchi wana haki ya kupata taarifa na rasilimali hizi ni mali ya wananchi na Serikali imepewa dhamana ya kuzishika rasilimali hizo, hivyo ni muhimu kwa wananchi kujua na kuelewa ni nini kinafanyika kwenye rasilimali zao na Serikali yao imeingia kwenye mikataba ya aina gani.

Pia upepo wa kiuchumi unaonesha kwamba sekta ya Uziduaji inakua na kuendelea kutokana na teknolojia mpya na makampuni ya uwekezaji yanazidi kuja nchini kwa wingi. Hivyo kutokana na ukuaji huo ni vizuri kuelewa ni mikataba ya aina gani Serikali ya Tanzania inaingia na makampuni hayo ya uwekezaji.

Meneja wa Programu kwenye chama cha wanasheria Tanganyika (TLS), Steven Msechu anasema: “Uwazi wa mikataba kwenye sekta ya Uziduaji ni kitu ambacho wananchi wamekuwa wakidai kwa muda mrefu na tumeona ni kitu muhimu kuwepo kutokana na sababu kadhaa.”

Sekta ya uziduaji ni sekta yenye rasilimali ambazo zinakwisha na ni sekta ambayo katika utekelezaji wake huharibu sana mazingira hivyo ni vizuri kuweka tozo stahiki itakayosaidia baadaye na ili wananchi waifahamu tozo iliyopo ni lazima kuufahamu mkataba unasemaje.

Sekta ya uziduaji imekuwa ikiendeshwa kwa usiri mkubwa na pamoja na kuwepo kwa madini na mafuta kwa kiwango kikubwa lakini bado umasikini ni changamoto kubwa sana.

Kutokana na hali hii ndiyo maana ndiyo maana ni vizuri kujua kwanza mikataba inasemaje na kwa kufanya hivi itakuwa rahisi kuishauri Serikali juu ya nini cha kufanya au kurekebisha.

Thamani ya mkataba haipo kwenye fedha tuu maana yenyewe hubeba fedha na hasara zinazoweza kujitokeza, ikiwemo hatua za kupunguza uharibifu wa mazingira na haki ya uwazi.

Ni msukumo mzuri kwa Serikali kuhakikisha wanaingia kwenye mikataba yenye manufaa kwa wananchi ambao kimsingi ndiyo wamiliki wa rasilimali za taifa.

Uwazi wa mikataba ni njia mojawapo ya kuhakikisha pande zote zinafaidika kwenye shughuli za Uziduaji.

Tanzania ilipitisha sera ya uwazi na uwajibikaji katika sekta ndani ya sheria ya mwaka 2015 na dhumuni kubwa ni kuongeza uwazi na uwajibikaji katika sekta ya Uziduaji.

Sheria inaitaka Serikali kuweka mikataba wazi kupitia Waziri wa madini ambapo kamati ya madini hulazimika kumuhimiza waziri katika kuhakikisha anatekeleza jukumu hilo kwa manufaa ya wananchi.

Mpaka sasa ni miaka takribani 3 tangu sheria ipitishwe lakini mikataba bado haijawekwa wazi. Kutokana na utafiti uliofanywa na HakiRasilimali unaonesha kwamba Wizara ya madini ipo kwenye hatua nzuri ya kuhakikisha mikataba inawekwa wazi.

Asasi za kiraia kupitia mtandao wa HakiRasilimali zinapendekeza kwamba mchakato mzima wa uandaaji wa mikataba uwe wazi, wa haki na wenye ufanisi. Kutokea kwenye hatua za upangaji, utoaji wa zabuni, ugawaji linganifu, na utoaji wa mikataba hadi utekelezaji.

Hivyo wananchi wanashauriwa kuendelea kudai taarifa kuhusu utayarishwaji wa mikataba kwa umma, muundo wa uendeshaji shughuli, mapato, tathmini ya matokeo ya mazingira na mgawanyo wa mapato yanayotokana na shughuli za sekta ya madini, mafuta na gesi.
 
Kama wananchi! Kuna kitu tunapaswa kuwafunza hawa viongozi, nacho ni "UWAJIBIKAJI" vinginevyo wataendelea kuvunja katiba wapendavyo na watakavyo ila vunja wewe raia sasa!! Jasho litakutoka!
 
Ukiona tunafichwa ujue wakubwa wana maslahi yao humo.. Ilianza awamu zilizopita nilitegemea awamu hii wawe wazi kwani tumeambiwa tunapambanana ufisadi

Sasa kama hata uwakilishi wa wananchi tunafichwa, wabunge wetu wanatuwakilisha kisiri siri bila sisi kuona uwakilishi wao tutajuaje ufanisi wao? how do we measure their performance?
 
Maoni yangu:

Si kama watanzania ni wajinga kama watunga sera wanavyoweza kuwadhania, ila wanaopewa fursa ya kuendesha nchi wakishapata madaraka wanajisahau sana. Hizi dharau za viongozi wetu ambao wamegeuka watawala ndo zimetufikisha hapa.

Mikataba ikiwa wazi tena kwa lugha yetu ya Taifa (Kiswahili) itapelekea kila mtanzania kutambua ananufaikaje na rasilimali zinazopatikana nchini mwake.

Ni upuuzi mkubwa kwa waliopata mamlaka kutuchukulia poa na kuendelea kuchezea rasilimali zetu kwa kificho na kushibisha matumbo yao na jamaa zao wakidhani mwisho wao wana maamuzi yao!

Kwa leo naishia hapa
 
Naunga mkono hoja ya takwa hili la kisheria ambalo linaimarisha ulinzi wa rasilimali zetu bila kuathiri usalama na faida za kiuchumi kwa nchi yetu.
 
Back
Top Bottom